Soma zaidi hapa...
Songwe. Changamoto za maisha ndizo zilizomsukuma kijana, Adam Zacharia, maarufu kama mhandisi wa mtaani, kubuni mashine mbalimbali kwa kutumia vyuma chakavu, kutengeneza mashine za kuchakata mazao na vipuri vya magari, huku akiwapa mafunzo ya ujuzi wa vitendo zaidi ya vijana 200.
Mbali na kuchakata mazao, Zacharia pia huongeza thamani ya mabaki ya mazao ya kilimo, kwa kutengeneza chakula bora cha mifugo pamoja na madawati na viti vya shule.
Licha ya kuishia elimu ya msingi, ameonyesha kuwa kipaji, ubunifu na uvumilivu, vinaweza kubadili maisha ya mtu na kutoa suluhisho kwa changamoto zinazokabili sekta za kilimo na magari.
Mzaliwa wa Mkoa wa Njombe ambaye sasa anaishi Mpemba katika Mji wa Tunduma, Mkoa wa Songwe, Zacharia anaendesha karakana yake umbali wa mita chache kutoka Barabara Kuu ya Tanzam inayounganisha Tanzania na Zambia, upande wa kushoto kuelekea Mkoa wa Mbeya.
Nje ya karakana hiyo kuna mfano wa helikopta aliyoutengeneza kwa ubunifu miaka kadhaa iliyopita, ukiwa ushahidi wa uwezo wake wa kubuni.
Ingawa hakufanikiwa kuukamilisha mradi huo kutokana na ukosefu wa fedha, ubunifu huo ulimpatia umaarufu mkubwa ndani na nje ya Tanzania. Akizungumza na Mwananchi, Zacharia alisema alihamia Tunduma mwaka 2002 akitokea Mkoa wa Iringa kutafuta maisha.
Alisema tangu alipofika eneo hilo alijikita katika kazi za ufundi mitambo na utengenezaji wa mashine, akilenga kutatua changamoto zinazowakabili wakulima.
Alieleza safari yake kuwa haikuwa rahisi kwani alipitia vipindi vya kukata tamaa kutokana na kufanya kazi katika mazingira magumu, bila mtaji wa kutosha na kwa kutegemea nguvu kazi nyingi za mikono kutengeneza mashine.
“Nilianza bila mtaji wala vifaa vya kisasa. Nilikuwa na elimu ya msingi pekee, lakini sikuacha kuamini uwezo wangu,” anasema.
Katika hatua za mwanzo, anasema alitengeneza mashine kwa kutumia vyuma chakavu, ingawa hazikuwa na ubora wa kuridhisha.
Hata hivyo, hakukata tamaa na aliendelea kuboresha kazi zake hadi akafanikiwa, jambo lililomfanya kuwa tegemeo la wananchi. Ili kuongeza kipato, Zacharia alibuni gereji inayotembea, ubunifu uliomjengea kujiamini na kumtangaza ndani na nje ya nchi.
Alisema mapato aliyoyapata kupitia huduma hiyo, ndiyo yaliyomwezesha kuendesha maisha yake na kuendelea kufadhili jitihada za kutengeneza mashine za kuchakata mazao.
Mafanikio yalianzia shambani
Zacharia alisema hatua kubwa ya mafanikio ilianza baada ya ofisa kutoka Idara ya Maendeleo ya Jamii kuona mashine yake ya kuchakata mazao inayotumia injini ya dizeli na iliyotengenezwa kwa vyuma chakavu ikifanya kazi shambani, ndipo akamfungulia milango ya fursa mbalimbali.
Mafanikio makubwa zaidi yalikuja mwaka 2019 aliposhiriki shindano la wabunifu lililoandaliwa na Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech) jijini Dodoma.
Akiwa mshiriki kutoka sekta isiyo rasmi, Zacharia alishindana na wabunifu mbalimbali kuanzia wenye elimu ya msingi hadi wahitimu wa vyuo vikuu.
“Nilieleza namna ubunifu wangu unavyosaidia kutatua changamoto za wakulima na kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvuna. Baada ya kueleza changamoto nilizokuwa nazo, Costech walinipatia vifaa vya kisasa vyenye thamani ya Sh94 milioni. Hapo ndipo safari mpya ilipoanza,” alisema.
Baada ya kupata mashine za kisasa, Zacharia alisema uwezo wake wa uzalishaji uliongezeka kwa kiwango kikubwa na kuvutia wateja kutoka Tanzania, Zambia na Malawi.

Vijana zaidi ya 200 wanufaika
Zaidi ya vijana 200 wamepata mafunzo katika kituo chake, huku wengi wao wakianzisha karakana zao binafsi.
Anasema mafanikio hayo pia yamemwezesha kulipa kodi, kuzalisha ajira na kuongeza tija katika sekta ya kilimo kwa kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno.
Kwa mujibu wa Zacharia, mashine anazotengeneza zina uwezo wa kuchakata tani moja ya mahindi ndani ya saa moja kwa kutumia takribani lita moja ya dizeli, jambo linalopunguza gharama na muda wa uzalishaji kwa wakulima.
“Lengo si kuchukua nafasi ya kazi za mikono, bali kutoa teknolojia nafuu inayopunguza upotevu wa mazao,” anasema.
Hata hivyo, anasema changamoto kubwa inayomkabili ni ukosefu wa mtaji.
“Mahitaji ya mashine ni makubwa sana Songwe na hata nchi jirani za Malawi na Zambia, lakini ukosefu wa fedha unazuia kuongeza uzalishaji.”
Pia aliiomba Serikali kurahisisha taratibu za usajili wa bidhaa ili wabunifu wa ndani waweze kuziingiza sokoni kwa urahisi zaidi.
Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo na Uhawilishaji Teknolojia wa Costech, Dk Erasto Mlyuka, anasema Serikali imetenga zaidi ya Sh4 bilioni kupitia Samia Innovation Fund kwa ajili ya kuwawezesha wabunifu wa ndani wanaochochea ukuaji wa uchumi.
Anamsifu Zacharia kwa mchango wake, akieleza kuwa Costech ilishirikiana na Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Kampasi ya Songwe, kuboresha ubunifu wake ili kufikia viwango vya kimataifa vya kisayansi.
| # | Наименование новости | Тональность | Информативность | Дата публикации |
|---|---|---|---|---|
| 1 | Ndejembi awakuna wadau, apewa angalizo | 0 | 10 | 27-08-2026 |
| 2 | Kinachofuata kwa Dk Nchimbi | 0 | 10 | 27-08-2026 |
| 3 | Sinza: Kutoka makazi, bata hadi kitovu cha biashara | 0 | 10 | 27-08-2026 |
| 4 | Mapato Stendi ya Magufuli yapaa | 0 | 10 | 27-08-2026 |
| 5 | Bunge kumthibitisha Ndejembi leo | 0 | 10 | 28-08-2026 |
| 6 | Utata ukomo umakamu wa rais wa Nchimbi, wanasheria watofautiana | 0 | 8.4 | 27-08-2026 |
| 7 | UCHAMBUZI WA MJEMA: Tusijidanganye, tunahitaji maandalizi haya kabla ya 2030 | 0 | 18.33 | 27-08-2026 |
| 8 | UWT: Hakuna mwanachama aliye juu ya CCM | 0 | 10 | 28-08-2026 |
| 9 | Chanzo ghorofa kupigwa mnada kwa mkopo wa Sh10 milioni | 0 | 5 | 20-07-2026 |
| 10 | Uso unavyoweza kuonyesha dalili za figo kuanza kuathirika | 0 | 10 | 25-08-2026 |